Omog ametoa msimamo mkali. - Erick Picson Media

Erick Picson Media

Mkali wa Matukio na Habari za Burudani

Breaking

Tuesday 10 October 2017

Omog ametoa msimamo mkali.

KOCHA wa Simba, Joseph Omog amesisitiza kwamba tangu anasaini mkataba alifahamu atakuwa chini ya presha kubwa Msimbazi kutokana na ukubwa wa klabu hiyo na wingi wa mashabiki.

Omog ameenda mbali zaidi na kusema kwamba, atapendelea kama akiona shabiki mmoja ambaye amejitokeza na kumpinga kwa hoja zenye mashiko kuwa timu haichezi vizuri au kuna kitu gani aambacho hakiendi sawa.

Amesisitiza kuwa kelele na presha zinazopigwa pembeni ni hali ya kawaida kwenye mashindano ndio maana amewaambia wachezaji wake watulize akili wafanye kazi na hilo ndio sababu wanaongoza ligi.

“Tangu nakubali kuifundisha Simba nilitambua kuwa nitakuja kukutana na kelele za mashabiki tena zaidi ya hizi ambazo wanasema wakati huu,” alisema kocha huyo wa zamani wa Azam.

Omog, ambaye amewahi kuinoa kwa mafanikio AC Leopards ya DR Congo alisema; “Nimekuja kufanya kazi na ndio maana tumeanza msimu vizuri na tunaongoza ligi hadi sasa, kwa upande wangu naona hao mashabiki wanapiga tu kelele wala hawana sababu ya msingi ambayo inawafanya waongee maneno ambayo si mazuri.

“Natoa ruhusa kama kuna shabiki wa Simba mwenye pointi za msingi ambazo zinamfanya kuongea maneno mengi juu ya maendeleao ya timu msimu huu ajitokeze, anikosoe kwa hoja,” alisema.
“Tumejipanga kuhakikisha tunafanya vizuri msimu huu na kwa kikosi nilichokuwa nacho nina imani nitatimiza lengo letu kuu,” alisema Omog ambaye nahodha wake ni Method Mwanjali wa Zimbabwe.

Mghana wa Simba afunguka
Straika Mghana Nicholas Gyan aliyenunuliwa kwenye klabu ya Ebusua Dwarfs amedai presha iliyoko Msimbazi ni kubwa kuliko alikotoka, lakini hata viwanja vingi ni chakavu hivyo hawezi kufanya mambo yake kama alivyotarajia.

“Timu ya Simba ni kubwa ina presha ya mashabiki ambayo nilikuwa sipati mara kwa mara kule kwetu Ghana, lakini hapa kila mechi nakutana na presha, ligi ya Ghana si ya kutumia nguvu kama ilivyo ligi ya hapa kwani, wachezaji ambao tunakutana nao wanakuwa wanakamia na mimi nilikuwa sijazoea kucheza kwa aina hiyo,” alisema.

“Ukiondoa viwanja vya Dar es Salaam, vingine vimekuwa vikinipa wakati mgumu wa kucheza kwa kuwa, eneo la kuchezea si zuri kabisa tofauti na kule kwetu huwa tunatumia viwanja ambavyo ni vizuri sehemu ya kuchezea,” alisema.

“Nimeshaanza kuzoea mazingira mapya, ila ninachoomba mashabiki wa Simba ni kunipa muda, nikiweza kufunga hata katika mechi moja tu, huo ndio utakuwa muendelezo wangu kwani, natambua mashabiki wa Simba wanatamani kuniona nafunga mara kwa mara.

“Moja ya malengo yangu katika timu ya Simba kuwa ni miongoni mwa wafungaji bora katika miaka miwili yote nitakayokuwepo hapa,” alisema Gyan.
Lakini, Mwanjali aliongeza kwamba; “Kwa hiyo tunatambua ugumu uliokuwa mbele yetu na tumejiandaa kuikabili ili kuweza kupata matokeo ya ushindi katika michuano yote ambayo tuliyopo msimu huu.”

No comments:

Post a Comment