Tshishimbi ameipa moyo yanga - Erick Picson Media

Erick Picson Media

Mkali wa Matukio na Habari za Burudani

Breaking

Monday 15 January 2018

Tshishimbi ameipa moyo yanga

BAADA ya kuondolewa kwenye hatua ya nusu fainali ya Kombe la Mapinduzi, kiungo mkabaji wa Yanga, Papy Kabamba Tshishimbi, amewapandisha mzuka mashabiki wa timu hiyo kwa kuwaambia hasira zao zote zinarudi katika Ligi Kuu Bara.

Yanga iliondolewa na URA ya Uganda katika michuano hiyo, kwa kufungwa kwa njia ya penalti 5-4 baada ya dakika 90 kumalizika kwa suluhu.

Timu hiyo, jana Jumapili ilianza maandalizi ya ligi kuu katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam chini ya Kocha Mkuu Mzambia, George Lwandamina aliyerejea nchini hivi karibuni.

Keshokutwa Jumatano, wanatarajiwa kucheza dhidi ya Mwadui FC jijini Dar es Salaam.

Kiungo huyo raia wa DR Congo, alitoa kauli hiyo kupitia moja ya akaunti zake za kijamii akiwataka mashabiki wa timu hiyo kutokata tamaa baada ya kulikosa Kombe la Mapinduzi na badala yake kuelekeza nguvu katika ligi kuu ili wautetee ubingwa wao.

Tshishimbi alisisitiza kuwa, mapambano yanaendelea licha ya kuondolewa katika michuano hiyo huku akiahidi kufanya vema katika mechi zao zijazo za ligi kuu.

“Niwaambie mashabiki wa Yanga kuwa, bado mapambano yanaendelea katika ligi kuu baada ya kutofanya vizuri katika michuano iliyopita,” aliandika Tshishimbi.

Mcongo huyo, tangu amerejea katika timu hiyo, ameonekana kutoa msaada mkubwa kutokana na kiwango kikubwa ambacho amekuwa akikionyesha ndani ya uwanja.

Tshishimbi hivi karibuni alikuwa nje ya uwanja akiuguza majeraha ya kifundo cha mguu kabla ya kurejea hivi karibuni katika mechi ya Kombe la FA wakati timu hiyo ilipocheza dhidi ya Reha FC

No comments:

Post a Comment