Njombe mji kuuvaa mziki wa Okwi - Erick Picson Media

Erick Picson Media

Mkali wa Matukio na Habari za Burudani

Breaking

Friday 20 October 2017

Njombe mji kuuvaa mziki wa Okwi

Vinara wa Ligi Kuu Bara, Simba itawakaribisha jijini Njombe Mji kwenye Uwanja wa Uhuru leo, Jumamosi, wakati Yanga itakuwa ugenini Shinyanga kuwakaribi wenyeji wao Stand United.

Simba wenye pointi 12, inajua matokeo yoyote mbali ya ushindi yatawaondoa katika usukani wa ligi hiyo kutokana na ushindani mkali kutoka kwa Azam, Mtibwa Sugar, Yanga, Singida United na Prisons zote zinaweza kukalia kiti hicho cha uongozi ligi hiyo.

Njombe Mji iliyopanda daraja msimu huu itashuka kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam wakiwa tayari kukabiliana na kimbunga Okwi.

Mshambuliaji Emmanuel Okwi tayari ameshafunga mabao saba yote akifunga kwenye Uwanja wa Uhuru hivyo kuna uwezekano mkubwa wa kuendelea na rekodi hiyo leo.

Mganda huyo pia analengo la kurudia mafanikio yake ya msimu 2011-12 alipoiongoza Simba kutwaa ubingwa kwa mara ya mwisho pamoja na kuwa mfungaji bora wa ligi msimu huu.

Kocha wa Njombe, Mrage Kabange ambaye ni mwanachama na mchezaji wa zamani wa Simba aliyekabidhiwa timu baada ya Hassan Banyai kubwaga manyanga amekuwa na rekodi nzuri na hajapoteza mchezo wowote jambo ambalo limempa hali ya kujiamini kuwa anaweza kufanya vizuri pia dhidi ya Simba ambayo haijashinda taji la VPL kwa miaka mitano sasa.

"Simba ni timu kubwa, ina kikosi kipana na ni ngumu kusema utamkaba nani ili kuwazuia. Pamoja na yote nimekuwa na rekodi nzuri, tumejiandaa kuilinda, saikolojia ya wachezaji iko vizuri kupambana," alisema Kabange.

Mchezo mwingine ni mataji wa Singida, timu ya Singida United watakuwa ugenini kuwavaa Ndanda kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara.

Kocha wa Singida United, Hans Van Pluijm alisema licha ya timu yake kupewa nafasi kubwa ya kushinda mchezo huo anaitazama Ndanda kama timu ngumu kucheza nayo hasa inapokuwa nyumbani.

Kocha wa Ndanda, Malale Hamsini alisema; "Singida United ni timu nzuri, lakini sisi ni wazuri zaidi. Tumeona namna wanavyocheza mechi zao za nyuma, bado hawajawa na kasi kubwa ya kufunga na ndiyo sababu wameshinda kwa mabao machache, hili linatupa imani ya kushinda."

Mabingwa mwaka 2013, Azam wenyewe watakuwa ugenini leo Jumamosi kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, kuwakabili wenyeji wao Mbao

Azam imeingia Mwanza ikiwa na kumbukumbu ya kipigo cha mabao 2-1 msimu uliopita hivyo wanahitaji ushindi ili kulipa kisasi.

Mechi nyingine leo Jumamosi, Mtibwa Sugar itacheza na Prisons, Lipuli itacheza na Majimaji wakati Mbeya City ikiwa wenyeji wa Ruvu Shooting.

Kesho, Jumapili, Mabingwa watetezi Yanga watacheza na Stand United kwenye Uwanja wa Kambarage, Shinyanga wakiwa na kumbukumbu ya kipigo cha bao 1-0 msimu uliopita.

No comments:

Post a Comment